Monday, July 8, 2013

HUDUMA YA TRENI LA JIJI KESHO HAIPO....KICHWA KIMOJA NI KIBOVU

Uongozi wa Kampuni ya Reli Tanzania –TRL unasikitika kuwataarifu wananchi na wakazi wa jiji kwa jumla kuwa huduma ya treni ya jiji haitokuwepo kwa muda wa siku 2 kuanzia leo Julai 8, 2013 kutokana na hitilafu kubwa katika  kichwa kimojawapo cha treni hiyo.

Uamuzi huo unatokana na sababu za kiufundi unaosimamia uendeshaji wa huduma hiyo jijini.

Kwa utaratibu huduma hii huendeshwa kwa kutumia vichwa vya treni vitatu ambapo viwili uhudumia moja kwa moja na cha tatu huwa cha akiba .

 Kuanzia siku ya Jumamosi ambapo huduma haikuwepo, kichwa cha  tatu kiligundlika kuhitaji matengenezo makubwa na kupelekwa katika karakana yetu ya Morogoro.



Kutokana na utaratibu tulioainisha hapo awali kukosekana kichwa cha dharura ’standby’ kunalazimisha tusitishe huduma kwa muda. Hata hivyo Wahandisi na Mafundi wa Karakana yetu Kuu Morogoro wanatarajia kukamilisha kazi hiyo kabla ya siku ya Jumatano na hivyo kutoa fursa huduma hiyo kuanza tena siku ya  Jumatano Julai 10, 2013.

Uongozi wa TRL unawaomba radhi wakazi wa Jiji na kuwataka kuwa na uvumilivu wakati huu wa ukarabati  kichwa cha treni unaoendelea na kwamba muda sio mrefu Wanareli wa TRL  watafanya kila linalowezekana kuirejesha huduma hii walioizoeya.

Tamati
Imetolewa na Afisi ya Uhusiano ya TRL kwa Niaba ya
Mkurugenzi Mtendaji ,
Mhandisi Kipallo Aman Kisamfu
Dar es Salaam,
Julai 08, 2013.