Serikali kupitia Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii imesema sekta ya Afya inaupungufu wa madaktari kwa asilimia 47 kwa kada zote za Afya, hivyo imeajiri wataalamu wa Afya wakiwamo madaktari waliopo katika mazoezi kwa vitendo waliosimamishwa kutokana na mgomo wa madaktari mwaka jana.
Hayo yalisemwa jana na Msemaji wa Wizara hiyo, Nsacris Mwamwaja wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mkakati wa Serikali katika utekelezaji wa utoaji huduma za afya kutoka ngazi ya kijiji hadi Taifa.
Alisema madaktari wote waliokuwa katika mazoezi kwa vitendo na waliomaliza mafunzo yao (Interns) waliosimamishwa mwaka jana kutokana na kushiriki katika mgomo wa madaktari na wao wamejumuishwa katika ajira hizo mpya.
Alisema katika ajira hizo mpya, Wizara imeajiri madaktari 473 lengo likiwa ni kuboresha huduma za afya hapa nchini.
Mwamwaja alifafanua kuwa madaktari wa mafunzo kwa vitendo wote waliosimamishwa kazi mwaka jana na Wizara walirudishwa kazini baada ya Baraza la Madaktari Tanganyika (MCT) kuwaita na kuwapa adhabu ambazo walizitumikia.
Aliongeza kwasasa kada zote za afya zinawahudumu wa afya kwa kiwango cha asilimia 53 tu.
“Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii kwa kuzingatia Mpango wa Maendeleo ya Afya ya Msingi (Mmam-2007/17) imejikita katika kutekeleza maeneo yakiwamo Rasilimali watu,ujenzi na ukarabati wa vituo vya huduma za Afya,” alisema Mwamwaja
Mwamwaja alisema kwa mwaka wa fedha 2012/2013 Wizara ilipata kibali cha kuwapangia vituo vya kazi wataalam wa afya 8,869 ikijumuisha Halmashauri,Tawala za Mikoa,Hospitali za Mashirika ya kujitolea,Wizara.
Alisema wataalam hao ni wauguzi,wateknolojia viungo bandia, wateknolojia mionzi, wateknolojia macho, wateknolojia maabara, wateknolojia dawa, pamoja wasaidizi afya mazingira.
Zingine ni Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH),Taasisi ya Saratani Ocean Road, Hospitali ya Rufaa Bugando na CCBRT.
Mwamwaja alisema katika kuongeza watumishi wa kada ya Afya katika mamlaka mbalimbali za ajira mwaka 2008/09 waliajiri watumishi 5,241, 2009/10 watumishi 6,257 2010/11 watumishi 7,471 2011/12 watumishi 9,391.
Sekta ya Afya nchini imekuwa ikikabiliwa na matatizo mbalimbali ikiwamo migomo ya madaktari, ikiwa Agosti mwaka jana madaktari waliokuwa mafunzoni wapatao 229 walifukuzwa baada ya kutokea kwa mgomo wa madaktari ambao na wao walishiriki.