Thursday, August 15, 2013

WAATHIRIKA DAWA ZA KULEVYA WASAIDIWE",KIKWETE

RAIS Jakaya Kikwete ameiagiza Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii kupitia Kitengo cha Magonjwa ya Akili na Tume ya Kuratibu Udhibiti wa Dawa za Kulevya nchini, kuwasaidia waathirika wa dawa hizo.
Rais alitaka Wizara na tume hiyo, kushirikiana na Kituo cha Ushauri cha Pili Misana Foundation, ambacho kinawasaidia waathirika wa dawa hizo, ili kiwahudumie watu wengi zaidi nchini.
Alisema hayo juzi Ikulu Dar es Salaam, alipokutana na vijana walioachana na matumizi ya dawa za kulevya, ambao wamepata ushauri nasaha na usaidizi kutoka katika kituo cha Pili Misana kilichopo Kigamboni jijini Dar es Salaam.
“Jamii lazima ishiriki katika utatuzi wa jambo hili, ni tatizo kubwa na linamgusa kila mtu na inabidi wote tushiriki katika kulipiga vita,” alisema Rais na kumpongeza Misana na Zacharia Hans Pope, ambaye ndiye mfadhili wa kituo hicho.
Kituo hicho tayari vijana wapatao 203, ambao wamepatiwa huduma ya ushauri na kuachana na dawa za kulevya na kurudia katika shughuli zao za kimaendeleo.
Rais Kikwete amesema tatizo la dawa za kulevya ni la muda mrefu, lakini hapo awali lilikuwa halisikiki sana kwa sababu jitihada za kuzuia dawa hizo zilikuwa hazitangazwi wala kufuatiliwa.
“Sasa hivi juhudi mbalimbali za kupambana na dawa za kulevya zinatangazwa na kusikika na pia taarifa nyingi zinazohusu dawa za kulevya zinawekwa wazi kwa jamii,” alisema Rais na kueleza kuwa taarifa nyingi zinawekwa wazi na kutangazwa, ili kushirikisha jamii kupambana na tatizo hilo.
Vijana 35 kutoka katika nyanja mbalimbali za kitaaluma, elimu na kijamii na umri tofauti kutoka miaka 14 hadi miaka 53, walifika Ikulu juzi kuzungumza na Rais.
Kituo hicho kinahudumia watu wenye jinsia tofauti, wake kwa waume kutoka sehemu mbalimbali nchini. Rais Kikwete alisema Serikali inafanya jitihada kubwa za kusaidia vijana mbalimbali na bado itaendelea kutoa msaada huo, huku juhudi mbalimbali za kupambana na dawa hizo zinaendelea.