Wednesday, August 14, 2013

POLISI MABINGWA WA KUPIGA,KUJERUHI,KUUA NA KUKANUSHA KWA NGUVU ZOTE..."

HUU ndio mtindo wa kawaida wa Jeshi la Polisi: kupiga, kujeruhi, kuua na kukanusha kwa nguvu zote.

Jeshi likiona makundi ya watu ambao lina mzio nao linapiga mabomu kuzusha tafrani; halafu linapiga virungu wale wanaowayawaya kutokana na macho kuwasha na kwa kuwa kila mtu huanza kukimbia hovyo ili kuokoa maisha zinapigwa risasi za moto. Waliojeruhiwa huchanganyikiwa hivyo huwa vigumu kujua risasi zimetoka wapi.
Hata pale maafa yanapomkuta mtu mmoja mmoja hujengwa mazingira iwe vigumu kujua ukweli hasa nani anahusika polisi au wahuni wa kisiasa.
Hivyo ndivyo polisi wamefanya mara zote Arusha, Songea, Morogoro na Iringa. Picha za video za mnato huonyesha polisi wakilenga kwa bunduki, kufyatua risasi, kujeruhi na kuua na siku inayofuata kamanda wa polisi wa mkoa au Inspekta Jenerali wa polisi au msemaji wa Jeshi la Polisi husoma taarifa kukanusha wao kuhusika.
Polisi watasingizia wananchi au vyama vya siasa kisha serikali itadaka uongo huo na kunga’ng’ania kuwa ni ukweli.
Uongo wa Jeshi la Polisi umeikifu jamii, unaifanya serikali ya Rais Jakaya Kikwete ionekane inanuka na chama tawala kinachoishi kwa mkono wa chuma wa polisi kimeoza.
Hata mwaka jana polisi walifanya hivyo dhidi ya wafuasi wa CHADEMA. Katikati ya maandamano yao mjini Morogoro, walitekeleza amri ya kupiga, kujeruhi na kuua na picha za video zilionyesha wakilenga na kisha kufyatua risasi ikamuua Ally Zona.
Kesho yake Kamanda Faustine Shilogile alikanusha na kwa uhodari akadai Zona alipigwa na kitu chenye ncha kali kilichorushwa kutoka kwa waandamanaji. Hapa alimaanisha CHADEMA ndio waliomuua lakini hadi leo hakuna mfuasi hata mmoja wa chama hicho aliyehojiwa mbali ya kushtakiwa.
Wakazi wa Nyololo, Iringa, wakasikia uongo mtakatifu wa Jeshi la Polisi ambao ulitetewa na serikali. Huko nako mikanda ya video ilionesha polisi wakimzingira, kumpiga, kumlipua na kumuaa Daudi Mwangosi na kesho yake polisi wakadai kuna kitu kilichorushwa kutoka mbali.
Hakuna mfuasi wa CHADEMA aliyenaswa isipokuwa polisi mmoja amefunguliwa mashtaka kukejeli wananchi.
Polisi hawajawahi kukiri kosa; wametetea mauaji yote na kwa bahati mbaya sana serikali ya CCM nayo imetetea uhalifu huo bila kujali inajimaliza au la.
Siku pekee ambayo serikali ilikataa taarifa ya polisi ni Januari 2006 wakati Rais Jakaya Kikwete akiwa bado mpya, na akifuata ilani ya uchaguzi ya chama chake juu ya kulinda raia.
Mwaka huo aliunda tume chini ya Jaji Kiongozi mstaafu, Mussa Kipenka, kuchunguza mauaji ya wafanyabiashara watatu wa Mahenge na dereva teksi mmoja jijini Dar es Salaam.
Tume iligundua kwamba vijana wale walikuwa wametekwa na polisi eneo la Sinza, wakapelekwa katika msitu wa Mabwepande ambako waliuawa kwa kupigwa risasi kama wahaini na wakaporwa madini na fedha.
Kesho yake polisi walidai wafanyabiashara wale walikuwa majambazi, walipora fedha katika kiwanda kimoja.
Mmiliki wa kiwanda alipoulizwa alikiri kuwepo tukio la wizi kiwandani lakini alikana kuwepo majibizano ya risasi kama polisi walivyodai.
Sijui nini kilitokea. Tangu polisi waumbuke katika tukio lile na kwa vile kila tume iliyoundwa, mfano bungeni, iliibua uoza mkali, JK hakuthubutu tena kuridhia kuunda tume kuchunguza tukio lolote lile dhidi ya polisi na amekuwa siyo tu akikubaliana nao bali pia kutetea uongo wao kila walipoua raia.
JK hakutaka kuunda tume tukio la mauaji yaliyofanywa na polisi Januari 5, 2011 dhidi ya wafuasi wa CHADEMA mkoani Arusha. Alikubaliana na taarifa ya polisi kwamba CHADEMA ndio waliokaidi amri na ndio waliohusika na mauaji ya watu watatu waliopigwa risasi.
JK hakukumbuka tukio la Zona kupigwa risasi maana polisi wanaonekana wazi wakilenga. Hakutaka kukumbuka tukio la Mwangosi, na kwa kushukuru kazi nzuri ya Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Iringa, Michael Kamhanda, aliyesimamia operesheni iliyosababisha kifo cha mwandishi huyo wa habari, alihamishiwa makao makuu ‘kula bata’.
JK anaona heri lawama kuliko kufedheheshwa na tume ya kuchunguza tukio la kutekwa, kuteswa kwa aliyekuwa mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari, Dk. Steven Ulimboka.
Polisi hawawezi kuendelea na kesi ya Mkenya Joshua Mulundi aliyesingiziwa mchana kweupe kumteka Dk. Ulimboka. Wamemfungulia kesi eti ya kuidanganya polisi. Wanachelewesha tu kumfikisha kortini ofisa usalama aliyehusika na waliomtuma lakini wanajua siku itafika hawatakuwa na uwezo kuzuia.
JK hakutaka kuumbuka hata kutekwa, kuteswa na kutobolewa jicho kwa mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri (TEF), Absalom Kibanda.
JK hataki na hataunda tume yoyote ya kuchunguza matukio ya watu waliorusha mabomu katika kanisa Katoliki la St. Joseph parokia ya Mfanyakazi Olasit mjini Arusha na pili siku chache wakati wa mkutano wa CHADEMA.
Ule moyo alioanza nao kazi ya urais umepotea; anakubaliana na kutetea uongo wa polisi kwa sababu anajua wanatumwa kufanya hivyo.
JK anajua kuwa polisi walikuwa wanamsaka kwa udi na uvumba Sheikh Ponda ili afunguliwe tena mashtaka ya uchochezi. Watanzania hawamuungi mkono Sheikh Ponda kwa uchochezi kama kweli ameufanya lakini mabomu ya machozi na risasi za nini wakati wa kumkamata?
Hakuna njia za kistaarabu za kumwita kiongozi huyo mwenye wafuasi maelfu kwa maelfu nchini. Polisi waliotumwa na wakubwa zao kutoka Dar es Salaam wameshindwaje kumpa Sheikh Ponda saa 12 au 24 au 36 au 48 ajisalimishe polisi Morogoro?
Ndivyo polisi wanavyowadhalilisha Godbless Lema, au Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe? Kwa nini polisi haohao wasitumie njia za kistaarabu badala ya kutanguliza mabomu na risasi kwa suala la Sheikh Ponda? Hata wakikanusha, nani atawaamini?
Tujiulize kwa nini hakukamatwa Zanzibar wala Dar es Salaam alikofanya mihadhara mingi, ila Morogoro ndiko wakubwa wanaagiza akamatwe? Polisi Zanzibar na Dar waliogopa nini?
Je, JK ameamua kuhamishia fikra za watu kwa wahamiaji haramu na majambazi ili kuvuruga fikra za watu wasifikirie uhalifu wa kisiasa unaofanywa na Jeshi la Polisi dhidi ya wananchi kwa maslahi ya CCM?
Imeandikwa na Lwitiko Sr

Source: Tanzania Daima